Wachambuzi na wadau mbalimbali wametoa maoni yao kuhusu Bajeti ya
Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/17, huku watumiaji wa huduma za fedha
kwa njia ya simu wakikumbwa na maumivu wa kodi.
Hiyo ni siku moja baada ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango
kuwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 20116/17.
Pamoja na mambo mengine, bajeti hiyo inapendekeza kuongeza ushuru wa
vinywaji baridi, maji ya juisi, vinywaji vikali, bia na sigara.
Pia itawagusa watumiaji wa M-pesa, Tigopesa, Airtel Money, Ezypesa kwa kukatwa Sh 280 kwa kila Sh 1000 watakayotuma.
Jana Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo), alisema hatua
hiyo ya Serikali kuendelea kutafuta kodi kwa kuzidi kuwaumiza wananchi
inakwenda kinyume na matarajio ya Watanzania wengi.
Alisema katika bajeti hiyo ya Serikali na ukusanyaji wa mapato yake,
katika kila Sh 1000 itakayokatwa kwa huduma kwenye ATM kuanzia Julai
Mosi mwaka huu, Sh 280 zitachukuliwa na TRA.
Zitto alisema hali hiyo pia itawakumba watumiaji wa miamala ya M-pesa,
Tigopesa, Airtel Money, Ezypesa ambalo ndilo kundi kubwa la Watanzania
wanaotumia huduma hiyo nchini.
Aawali kodi ya bidhaa ilikuwa asilimia 10 lakini kwa hatua ya kuongezwa
kwa kodi ya ongezeko la thamani kodi itapaa na kufikia asilimia 28.
Kwa mantiki hiyo, katika kila Sh 100 kodi ni Sh 28 na katika Sh 1000 kodi ni Sh 280.
Kutokana na hali hiyo kodi ya VAT hulipwa na mtumiaji wa mwisho ambaye
anatuma au kupokea fedha, hali ambayo itawaumiza watumiaji wa mwisho.
“Hivyo hivyo katika miamala ya M-pesa, Tigo pesa na kadhalika, katika
kila Sh 1000 itakayokatwa kwa huduma kwenye ATM kuanzia Julai 1, 2016,
Sh 280 zitachukuliwa na TRA,” alisema Zitto.
Alisema ameshangazwa na hatua ya Serikali kuongeza kodi ya VAT kwenye
utalii hali ambayo inaweza kusababisha Tanzania kupoteza watalii wengi
kwa washindani wake kwa sababu itaongeza gharama kwa watalii.
“Kama tunataka kutumia utalii kama kichocheo cha ajira ni vema kufikiria upya suala hili,” alisema.
Akizungumzia mapendekezo ya Serikali katika Sheria ya Kodi ya VAT ili
kutoza kodi bidhaa zinazotoka Zanzibar, alisema hatua hiyo inavunja
misingi iliyowekwa na sheria ya zamani ambayo ilifanana na ile za
Zanzibar.
“Ikumbukwe kuwa Sheria ya Kodi ya VAT ya 2014 ilivunja misingi
iliyowekwa ya sheria ya zamani ambayo ilifanana na ile ya Zanzibar.
Mapendekezo ya sasa yana madhara makubwa kwa Zanzibar kwa sababu hakuna
atayewekeza Zanzibar ili kufaidika na soko la Bara.
“Biashara nyingi zinazozalisha Zanzibar zitahamia Tanzania Bara.
Mapendekezo haya yanaweza kusababisha mgogoro kati ya pande mbili za
Muungano,” alisema.