Wakati
hali ikionekana si shwari visiwani Zanzibar baada ya kuwapo kwa madai
ya kutengana, kubaguana na kuharibiana mali, vyama vya CUF na CCM
vimetupiana mpira kwa kila kimoja kikimtuhumu mwenzake.
Mkurugenzi
wa Haki za Binadamu na Sheria (CUF) Wilaya ya Wete, Mwinyi Juma Ali
amesema kuwa chama hicho kinaheshimu misingi ya utawala bora na haki za
binadamu na kauli hizo hazina ukweli wowote.
Akizungumza
na mwandishi wa habari hizi jana ofisini kwake, Wete , Mwinyi alisema
chama hicho kinasikitishwa na vitendo hivyo hasa vya kufyekwa mashamba
na kusababisha hali ya umaskini kwa wananchi .
“Kusema
kuwa kitendo cha hujuma hizi kinasababishwa na CUF siyo kweli, kwani
chama chetu kinathamini na kuheshimu misingi ya utwala wa sheria na haki
za binadamu na hujuma hizi zinatuathiri hata sisi, ” alisema Mwinyi.
Hata
hivyo, jana Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba,
Omar Khamis Othman alisema hujuma hizo zinapangwa na kuratibiwa na
wafuasi wa CUF.
Othman
aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi baada ya kutembelea
shamba la mihogo na migomba, lenye ukubwa wa eka tano lililofyekwa.
Othman
alivitaka vyombo vya ulinzi kuhakikisha wahusika wanakamatwa na
kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kwani vitendo hivyo vinaweza
kusababisha uvunjifu wa amani.
Akizungumzia
hayo, Mkurugenzi wa CUF, Mwinyi alisema kwamba tangu tuhuma hizo zianze
kuelekezwa kwa wanachama wa CUF, hakuna hata mwananchama mmoja ambaye
amefikishwa mahakamani wala kutiwa hatiani na kuongeza huo ni msamiati
wa propaganda za kisiasa.
Kuhusu
migomo inayoendelea, alisema CUF haihusiki na masuala hayo, bali
imekuja baada ya viongozi wa Serikali kuwakatisha tamaa wananchi
kutokana na chuki zao binafsi
0 comments:
Post a Comment